Na Abel Shema.
Mkuu wa Mkoa wa Kagera Mhe. Fatma Mwasa ameipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Bukoba kwa kupata hati safi, na kuvuka lengo la makusanyo ya mapato ya ndani kwa mwaka wa fedha 2024/25 kutoka shilingi Bilioni 3.1 hadi Bilioni 3.4 sawa na asilimia 112 hadi kufikia Mei 31,2025.
Hayo yamesemwa katika kikao maalum cha baraza la madiwani la kujadili hoja za mdhibiti na mkaguzi mkuu wa serikali (CAG), kilichofanyika katika ukumbi wa Chemba Juni 16,2025.
Akizungumza mbele ya baraza la madiwani Mhe.Mwasa alisema;
‘’Mheshimiwa Mwenyekiti natambua kuwa Halmashauri yako katika ukaguzi wa hesabu za serikali 2023/24 imepata hati safi,niwapongeze sana kwa jitihada zenu ambazo zimeisaidia Halmashauri yenu kupata hati safi’’.
Mwasa alisisitiza kufanikiwa kupata hati safi ni rahisi, lakini kuendelea kushikilia nafasi hiyo ni kazi kubwa, hivyo aliwaelekeza waheshimiwa madiwani,mkurugenzi mtendaji na watumishi kujikita kikamilifu katika kusimamia sheria,taratibu na miongozo ya serikali ili kuendelea kupata hati safi na kupata fedha Zaidi za maendeleo.
Mh.Mwasa aliongeza kuwa vigezo vinavyotumika katika upimaji wa utendaji kazi wa Halmashauri ni pamoja na ukusanyaji wa mapato ya ndani ambapo kwa Halmashauri ya wilaya ya Bukoba ni ya kuridhisha kwani kufikia Mei 31,2025 tayari imevuka lengo la makusanyo ya mwaka huu wa fedha.
Katika hitimisho la hotuba yake RC Mwasa aliwataka watumishi kuzingatia matumizi ya mfumo wa ukusanyaji fedha yani TAUSI, huku akiitaka Halmashauri kuhakikisha inakusanya mapato yatokanayo na ushuru wa mabango na kodi za majengo.
Bujunangoma
Anuani ya Posta: P.O.Box 491 Bukoba - Kagera
Simu ya Mezani: 028-2220287
Simu ya Mkononi:
Barua Pepe: ded@bukobadc.go.tz
Hati Miliki 2018 Halmashauri ya Wilaya ya Bukoba.Haki zote zimehifadhiwa.